Tuesday, July 16, 2019

FURSA ZA UWEKEZAJI UKEREWE




KARIBU UWEKEZE UKEREWE
Ukerewe ni moja ya maeneo bora zaidi katika Mkoa wa Mwanza kuwekeza katika fursa nyingi ikiwemo Uzalishaji wa samaki, dagaa na mazao yote ya ziwani, uwekezaji katika kilimo hasa matunda kama machungwa, maembe na machenza, uwekezaji wa usafiri ziwani kwani Ukerewe ina jumla ya visiwa 38. Huduma zote muhimu kama elimu, barabara, afya na upatikanaji wa chakula ni wa uhakika. 
karibu Uwekeze Nasi!

Sunday, July 30, 2017

JAFO AIPONGEZA UKEREWE KWA UFANISI KATIKA MIRADI YA MAENDELEO

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Mb) akizungumza na watumishi kushoto kwake ni Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Estominh Chang'ah na Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya Frank S. Bahati na kulia kwakwe ni Mwenyekiti wa Halmashauri George Nyamaha na makamo Kalala Greygory.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Mb) amefanya ziara Wilayani Ukerewe kwa dhumuni la kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo ambapo ametembelea Hospitali ya Wilaya, vituo viwili vya afya ambavyo ni Nakatunguru na Muriti, mradi wa maji Lutare Chabilungo na miradi ya P4R ya mabweni, madarasa na vyoo katika shule za sekondari za Pius Msekwa na Bukongo na kishakuzungumza na watumishi wa halmashauri katika ukumbi mkubwa mikutano.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Mb) akikagua mitambo na akipokea maelezo kutoka kwa mkandarasi wa mradi wa maji Lutare Chabilungo
Naomba nishukuru sana Miradi mingi sana imefanya vizuri hongereni kwa kazi nzuri, nimetembelea mradi wa maji vijijini Lutare Chabilungo kazi imeenda vizuri na ninaamini tukisimamia mradi ule ipasavyo katika sehemu iliyobakia wilaya itakua na uwezo wa kupata maji vijijini kwa wastani wa 77% kutoka 55% hivyo usimamiwe vzuri mpaka mwisho. Alisema Jafo. Mradi unatekelezwa kwa bajeti ya Bilioni 7 ambapo mpaka sasa serikali imeshalipa Bilioni 5. 
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Mb) akimtwisha ndoo ya maji mama katika kijiji cha Lutare
Ametoa rai marekebisho yafanyike mapema na kama kuna mabomba yaliyo chini ya kiwango yasitumike ilikuiepushia Halmashauri gharama za kununua mabomba pindi mradi utakapo anza kazi. Amemuagiza injinia wa maji wilaya William Kahurananga kuhakikisha vijiji 13 vilivyo kwenye mradi vinapata maji.
Sekta ya afya imekua na changamoto ya upungufu wa dawa hivyo amemwagiza Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya Dr. Revocatus Cleophas kuhakikisha wananunua dawa kwa ajili ya kuwahudumia wananchi “Pesa zote za kununua dawa zitumike kununua dawa na sio vinginevyo” alisema Jafo. Katika hatua nyingine amefurahishwa na matumizi ya mfumo wa malipo hospitali ukiwa unafanya kazi katika hospitali ya wilaya. 

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Mb) akiwa ndani ya chumba cha upasuaji akipokea maelezo ya kutuo cha Afya Muriti
Akiwa katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri akizungumza nao amewataka watumishi wabadilike katika utendaji wa kazi maana “a business as usual” imekufa na amesema pamejengeka tabia ya watumishi kufanya kazi pekee zenye maslahi. Amewahimiza kuwepo na kipimo cha watumishi katika utendaji wa kazi na kuacha ubabaishaji. Hivyo tubadilike katika utendaji wetu wa kazi na tunaagana ni kwa uweledi gani tunatakiwa kufanya kazi.
Aidha Kupimana kazini kwa mfumo wa OPRAS system imekua haifanyiki ipasavyo katka maeneo mengi imekua ni ya (copy and paste) kama celebration form ya  harusi au zinafanyika pale wakaguzi au upandaji wa madaraja lakini katika sekta binafsi unafanya kazi na utendaji unapimwa hivyo watumishi wa serikali wanapaswa kubadilika na kuanza kuweka mpango kazi wa nini anatarajia kutekeleza lengo moja baada ya lingine na mkuu wa idara afanye hivyo na ikifika mwaka mwingine wa fedha uhakiki ufanyike kubaini malengo mliokubaliana yamefanyiwa kazi au la.
Wakuu wa idara wanaoshindwa kutimiza majukumu yao ipasavyo nafasi zao zijazwe na wengine kwani Halmashauri ina wataalamu wengi wazuri wenye elimu kuanzia shahada ya kwanza (Degree) na shahada ya uzamili (masters degree). “Lazima tubadilike”alisema Jafo.
Jafo alisisitiza kuwa tunapeana maelekezo ili tujirekebishe “ukitaka kuruka agana na nyonga”
Katika miradi ya elimu jafo alitembelea shule mbili za sekondari za pius msekwa na bukongo ambazo zililetewa fedha zaidi ya shilingi 500milioni kutekeleza ujenzi wa mabweni ya kulala wanafunzi mawili kwa kila shule, madarasa mannne kila shule na matundu ya vyoo.
Amempongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ukerewe Frank S. Bahati kwani miradi mingi imetekelezwa katika ubora unaotakiwa na amewataka kurekebisha baadhi ya changamoto ilikuiletea ukerewe maendeleo  

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo (Mb) akikata mlango katika shule ya Sekondari Bukongo.



Friday, July 28, 2017

Mabula afanya ziara kikazi Ukerewe

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Angelina Mabula(Mb) akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Ukerewe.
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Angelina Mabula(Mb) amefanya ziara ya kikazi Wilayani Ukerewe kwa lengo la kukagua utendaji kazi wa Idara ya Ardhi Halmashauri na kuzungumza na watumishi. Ambapo alipokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Estominh Chang’ah na kupokea taarifa ya Wilaya ambapo alielezwa kuwepo kwa changamoto ya ubovu wa injini ya kivuko cha abiria kinachobeba abiria kutoka eneo la Bugorola kuelekea kisiwa cha Ukara.

Katika hatua nyingine akipokea taarifa ya idara ya ardhi Naibu Waziri Angelina Mabula aliwataka idara iongeza nguvu katika shughuli zao za kila siku kwani hali ilivyo ya ukuaji wa mji na idadi ya watu inapanda kila siku, hivyo amewataka kuhakikisha upimaji wa ardhi unaendana na ukuaji wa mji na idadi ya watu ili kupunguza migogoro ya ardhi.
Mabula amewataka watumishi wa idara hiyo kuwa waadilifu na kufanya kazi kama inavyopaswa na alisikitishwa kutokuwepo na matumizi ya Mfumo wa ukusanyaji malipo ya ardhi wakati mafunzo yalikwisha tolewa.
Mabula ameagiza Elia Mtakama ambaye anakaimu Ukuu wa Idara ya Ardhi na misitu kusimama mara moja nafasi yake ya Afisa Ardhi Mteule wa Wilaya kwani hajaridhishwa na utendaji wake. “kuanzia sasa Mkurugenzi Mtendaji Wilaya Afisa Ardhi mteule Elia Mtakama hatakuwa tena mteule hivyo atafutwe afisa ardhi mwininge mwenye vigezo apewe kazi hiyo” alisema Mabula.
Mabula amesisitiza masijala ya ardhi iboreshwe na nyaraka zote zilizopo zinatakiwa zifanyie kazi kuwahudumia wananchi na kuwaondolea usumbufu.
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Angelina Mabula(Mb) akikagua masijala ya Ardhi, kulia ni Mkuu wa Wilaya Estominh Chang'ah, Kaimu Mkuu wa Idara ya ardhi Elia Mtakama na Kaimu Mkurugenzi Hellen Rocky.




Wednesday, May 10, 2017

RC Mongella amewataka wadau kushirikiana kuboresha elimu Wilayani Ukerewe

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. John V.K Mongela akizungumza katika mkutano wa wadau wa elimu Ukerewe, Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Mhe. Estominh Chang"ah, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ukerewe Frank Bahati, Mwenyekiti wa Halmashauri Mhe. George Nyamaha(kulia kwa RC) 
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. John Mongella amefanya ziara ya Siku tano (5) Wilayani Ukerewe kwa dhumuni la kukagua shughuli za Halmashauri na  miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa. Ili kuhakikisha sekta ya elimu inakua na mabadiliko ambayo yataleta ufaulu na mazingira mazuri ya wanafunzi kujifunza. Katika kuhakikisha hayo Mongella amefanya kikao na wadau wa elimu Wilayani Ukerewe ambapo amewaweka pamoja walimu wa kuu na wakuu wa shule zote, wenyeviti wa bodi za shule, maafisa elimu kata, maafisa tarafa, watendaji, wadau wa taasisi zisizo za kiserikali na wataalamu wa elimu ngazi ya mkoa katika ukumbi mkubwa wa mikutano wa Halmashauri.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. John V.K Mongela akizungumza katika mkutano wa wadau wa elimu Ukerewe, Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Mhe. Estominh Chang"ah(kushoto kwa RC), Mwenyekiti wa Halmashauri Mhe. George Nyamaha(kulia kwa RC) 
Mongella amewaasa walimu kuwa na nidhamu ya kazi na uadilifu kwani wao ndio chanzo cha kuwa na maendeleo kielimu pia wawe mfano wa kuigwa. “bodi za shule ziwajibike na zisaidiane na uongozi wa shule kudhibiti nidhamu za watoto mashuleni” alisema Mongella. Amepiga marufuku kuunda tume kwa mwalimu atakae mpa mimba mwanafunzi na kesi za aina hiyo zisiwe za muda mrefu.
Amaewataka kuwepo na usimamizi madhubuti wa fedha za elimu bila malipo kwa shule zote za msingi na sekondari na fedha za serikali hizo zitumike kwa kufuata sheria, kanuni, taratibu na miongozo na kuahidi kuleta timu yakukagua fedha hizo na namna zilivyotumika na zinavyotumika na amewataka kurudisha hela kama mtu amezitumia vinginevyo. Lengo kuu ni kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu bora kutokana na fedha za elimu bure na historia inaonyesha ukerewe inauwezo mkubwa wa kufanya vizuri.
Wadau wa Elimu Wilayani Ukerewe
Mongella amezitaka kamati za shule na vikao vya wazazi vifanyike kila robo na visiishie kuchangishana bali wazazi wa elimishwe katika maeneo ya kitaaluma na wote wawajibike na taarifa na ratiba zipelekwe kwa Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella ametoa agizo juu wa ujenzi wa vyoo mashuleni ambapo amesema kufikia mwezi agosti 30 pasiwe na shule yenye upungufu wa matundu ya vyoo, na matundu ya vyoo katika shule yaende sawa na idadi ya wanafunzi na walimu katika shule husika. “bodi ya shule na mkuu wa shule ambaye hatakua amejenga choo itavunjwa” alisema Mongella. Pia amesisitiza bodi za shule na menejimenti za shule zihusike katika ujenzi wa vyoo.
Pia alisikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili katika kupeleka mbale elimu wilayani ukerewe na moja ya changamoto ni migogoro ya ardhi mashuleni hivyo akatoa maelekezo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri kuhakikisha wanaanza mara moja upimaji wa ardhi katika shule ili kuepusha migogoro hiyo.
Mongella amewataka maafisa elimu kata wawajibike katika kufuatilia shule zilizopo katika kata yake na kuacha uzembe wa kutokutembelea shule. Wametakiwa kusisimamia mfumo wa elimu kwenye kata na watoto wote wanatakiwa kwenda shule waripoti mashuleni, na ametoa rai kazi kubwa ifanyike yakizalendo na hakuna kitakachotushinda. Amesisitiza elimu ni sekta nyeti tusaidiane tuisukume ili twende mbele na kufikia mafanikio.

Wadau wa Elimu Wilayani Ukerewe


Tuesday, April 25, 2017

Wavuvi Ukerewe watakiwa kufuata sharia na kanuni za Uvuvi sahihi ili kutohatarisha mazalia ya samaki.

Kisiwa cha Gana ni moja ya visiwa vinavyounda Wilaya ya Ukerewe ambapo shughuli kuu za kiuchumi katika Wilaya ya Ukerewe na visiwa vyake ni Uvuvi kwa kiwango kikubwa na kilimo, hivyo wavuvi wametakiwa kujihusisha na uvuvi unaofuata sheria, kanuni na taratibu kwani utasaidia kuongeza kipato cha wavuvi na pato la serikali kiujumla.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Frank S. Bahati akiwa ameshika samaki ambaye alikuwa akikaguliwa kama alifaa kuvuliwa.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Ukerewe Frank S. Bahati amefanya ukaguzi wa mialo katika kisiwa cha Gana na kujionea shughuli mbali mbali za uvuvi wa samaki na dagaa, ambapo alitembelea kukagua maeneo ya uvuvi na shughuli wanazifanya katika maeneo ya mialo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Frank S. Bahati na Afisa Uvuvi Abbubakar Murshid wakiwa wamebeba samaki ambaye alikuwa akikaguliwa kama alifaa kuvuliwa kutoka katika mtumbwi wenye barafu.
 Katika ziara hiyo Bahati aliambatana na Afisa Uvuvi wa Wilaya Abubakari Murshid ambapo walikagua vipimo au rula ya kupima samaki waliokidhi vigezo vya kuvuliwa, hivyo akawaagiza wavuvi wote wa samaki wanatakiwa kuwa na rula yenye vipimo sahihi ambazo hazipotoshi na mizani ziwe nzima. Na kwa yeyeto atakaye bainika kwenda kinyume na maelekezo atachukuliwa hatua za kinidhamu.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe akiteketeza zana za uvuvi haramu.
 Katika shughuli nyingine Bahati ameongoza idara ya Uvuvi na mifugo katika uchomaji wa zana za uvuvi haramu zilizokamatwa katika maeneo mbalimbali ya wilaya na kutoa tamko kuwa patakua na kikosi kazi cha wataalamu wa uvuvi na doria za uvuvi watakao kuwa wakiishi katika visiwa ili kuweza kuangalia kwa ukaribu shughuli za uvuvi ili kukabiliana na uvuvi haramu unaofanywa na watu wachache wasio penda kufuata na kutii sheria, kanuni na taratibu.
zana za uvuvi haramu zikiteketea kwa moto.







Visiwa Kumi Wilayani Ukerewe kupata Umeme.


Mkurugenzi Mkuu wa Rex Energy Bw. Francis Kibhisa akizungumza katika uzinduzi wa mradi wa umeme jua kisiwa cha Gana
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Bw. Frank S. Bahati akizungumza katika uzinduzi wa umeme jua kisiwa cha Gana.
Wananchi wanaoishi maeneo ya visiwani wilayani Ukerewe wanatarajia kunufaika na huduma ya nishati ya umeme. Nishati hiyo ya umeme jua inayowezeshwa na mwekezaji Rex Energy ambao unatakuwa ni moja ya kichocheo cha uchumi wa maeneo mengi ya visiwa katika wilaya ya  Ukerewe na hii ni baada ya kufanya uzinduzi wa mradi huo wa umeme katika kisiwa cha Gana, uliohusisha wananchi waliojitokeza kwa wingi kushuhudia tukio hilo lililoongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Frank S. Bahati na Mkurugenzi mkuu wa Rex Energy Francis Kibhisa ambaye ndio mwekezaji.

Uwekaji saini katika uzinduzi wa mradi wa umeme visiwani.
Utekelezaji wa mradi wa nishati ya umeme jua unatakuwa wa awamu mbili, ambapo awamu ya kwanza imeanza agosti 2016 na kukamilika  desemba 2017, ambapo miundombinu imefikia hatua nzuri na visiwa vitakavyo nufaika na awamu hiyo ni Gana, Bwiro, Kamasi, na Bulubi. Katika awamu ya pili mradi utakamilika mwaka 2018 ambapo na kunufaisha visiwa vya Kweru kubwa, Kweru mto,Siza, Bushingere, Izinga na Sizu.
Ukaguzi wa miundombinu inayotumika katika mradi wa umeme jua

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Frank S. Bahati ameshukuru Rex Energy kwa kuwekeza nishati ya umeme jua katika visiwa kumi vya Ukerewe. Kupatikana kwa umeme katika maeneo ya visiwa utasaidia kukuza uchumi hasa wa viwanda kwani ni adhma ya serikali ya awamu ya tano kuwa na uchumi wa viwanda. Umeme utawasaidia vijana kujishughulisha na kazi mbalimbali, pia mradi utakua msaada kwa shule,vituo vya afya na taasisi za kidini. Amewataka wananchi kuupokea kwa mikono miwili mradi na kushirikiana kuutunza kuhakikisha unakuwa msaada kwa vizazi na vizazi.
Kikundi cha ngoma kikiburudisha katika uzinduzi wa umeme jua Gana
Mkurugenzi mkuu wa Rex Energy Francis Kibhisa ameshukuru Serikali kuanzia Wizara ya Nishati na Madini, Rea na serikali ya Wilaya ya Ukerewe kwa kutoa ushirikiano wa kufanikisha mradi huo kuanza kufanya kazi katika visiwa vya Ukerewe, baada ya miezi miwili umeme utakuwa umewashwa. Baada ya mradi kuanza kazi kuna maeneo ambayo itashirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kuboresha maeneo makuu matatu ambayo ni Elimu na kuimarisha majengo ya shule na vyoo kama ambavyo wamesaidia ujenzi wa choo cha shule ya msingi Miti mirefu, Afya kuanzisha kituo cha afya au zahanati, usalama kuweka kituo cha polisi.
Moja ya miundombinu ya mradi wa umeme jua kisiwa cha Gana
 “Gharama za mradi ni bilioni 18 hadi 21 ambazo ni sawa dola milioni 9 hadi 11 za kimarekani” alisema Kibhisa. Mradi utakuwa wa manufaa zaidi kwa vijana wengi watapata mafunzo na kuajiriwa katika kazi mbalimbali za Rex Energy. Ametoa rai kwa watanzania kuwekeza ndani ya nchi kama alivyofanya yeye na kuwa maendeleo ya nchi yanaletwa na watanzania wenyewe na kutokata tama katika kusaidia serikali.
Umeme jua wa Rex Energy unatarajiwa kuwanufaisha wananchi zaidi ya 5000 na itavutia wafanyabiashara wengi kutumia fursa na kujiongezea pato na wametakiwa kushirikiana na mwekezaji kutunza miundombinu.